Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk Stergomena Tax amesema serikali inatarajia kukamilisha ujenzi wa nyumba 5,000 ambazo zimeanza kujengwa za wakazi wa Msomera wilayani Handeni mMkoa wa Tanga waliohama kwa hiari kutoka Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro ndani ya miezi sita kutoka sasa.
Dk Tax ameyasema hayo wakati alipofanya ziara ya kutembelea kuona maendeleo ya ujenzi wa nyumba hizo zinazojengwa katika Kijiji cha Msomera mkoani Tanga, akiongozana na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Geophrey Pinda.
"Lengo letu ni kuhakikisha kwamba nyumba 1,000 zinakamilika mwishoni mwa mwezi Oktoba 2023 na tutaendelea kuzikabidhi nyumba kadri zinavyokwisha, lakini nyumba 5,000 zinarajiwa kukamilishwa mwishoni mwa mwezi Machi 2024," amesema.