Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Nyani, ngedere, tumbili watishia uhai, usalama wa chakula

0241398c24bd9a3b889d164e7d289e06 Nyani, ngedere, tumbili watishia uhai, usalama wa chakula

Wed, 21 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

MAKUNDI makubwa ya nyani, ngedere na tumbili kutoka katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro na hifadhi jirani ya Kenya wamekuwa tishio kwa uhai wa watoto wakiwamo wanafunzi sambamba na kutishia usalama wa chakula na wanyama wafugwao wilayani Rombo.

Mkazi wa Kijiji Cha Mrere, Anaeli Kimaro, alisema wanyamapori hao pia wamekuwa wakiiba watoto na kukimbia nao katika miti, jambo ambalo limezidi kuhatarisha usalama wa watoto.

Akizungumza mbele ya Mbunge wa Jimbo la Rombo, Profesa Adolf Mkenda na Waziri wa Maliasili na Utalii, Damian Ndumbaru aliyekuwa katika ziara wilayani humo, mkazi huyo alisema, katika moja ya matukio ya kutishawanyama hao walimuiba mtoto na kukimbilia juu ya mti.

"Wanachukua hadi watoto wetu... mmoja alichukuliwa hadi juu ya mti, tulimuokoa kwa shida, jambo hili linatutishia sana serikali itusaidie kwa kuwa tunapata shida," alisema Kimaro.

Akiwasilisha kero hiyo kwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Damian Ndumbaru, Mbunge wa Rombo, Profesa Mkenda, alisema maeneo ya vijiji mbalimbali yamevamiwa na wanyamapori hao na kuleta uharibifu katika mazao.

Alisema nyani, ngedere na tumbili licha ya kuharibu mazao ya wakulima pia wamekuwa wakishambulia na kula wanyama wafugwao kama mbuzi, kondoo na kujeruhi watoto hali inayohatarisha usalama wao hususani wanafunzi.

"Wanyama hawa wamekuwa wakileta madhara kwa wananchi hasa wakulima; wamevamia mashamba na wengine wanakula mbuzi, jambo hili ni hatari na lazima itafutwe njia ya kuwafukuza kwa usalama bila kuwadhuru," alisema.

Diwani wa Kata ya Kitangara Mrere, Venance Maleli aliiomba serikali kuwasaidia wananchi kuwafukuza kwani wanaharibu madhara kwa watu, mifuigo na mazao ya chakula.

"Wanyama hawa wamekuwa wakifuatana kwa makundi kati ya 100 hadi 200 na wananchi wamekuwa wakiwafukuza bila mafanikio, wanaharibu mazao katika mashamba... Tunawafukuza wanakimbilia kwenye miti mirefu na kurejea tena," alisema Maleli.

Akijibu kilio cha wananchi hao, Waziri Ndumaru alisema wanyama hao hawawezi kuuliwa kutokana na kutegemewa katika shughuli za utalii na kwamba serikali itafanya mpango bora wa namna ya kuwaondoa.

"Naagiza Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (Tawa) kuwafukuza wanyama hawa na kuwarudisha katika hifadhi na mbuga za wanyama ili kuondoa kero na usumbufu kwa wananchi na kufanya msako wa mara kwa mara," alisema.

Chanzo: www.habarileo.co.tz