Arusha. Wachimbaji wawili wa madini ya Ruby yanayochimbwa Wilayani Longido Mkoa wa Arusha wamefariki dunia baada ya kufunikwa na udongo wakati wakichimba.
Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo, Decemba 8, 2019 katika mgodi wa Mundarara Ruby Minning Ltd unaomilikiwa na Rahimu Mollel.
Kamanda wa Polisi Mkoa Arusha, Jonathan Shana akizungumza na Mwananchi amekiri kupokea taarifa za vifo hivyo.
“Ni kweli kuna wachimbaji wawili wa madini ya Ruby wamefariki wakiwa wanachimba na hadi sasa Ofisa upelelezi wa wilaya hiyo yupo eneo la tukio,” amesema Shana.
Amesema bado majina ya waliokufa hayajajulikana na uchunguzi ukikamilika taarifa rasmi itatolewa.
Kamanda Shana amesema pia inachunguzwa kama vijana hao walikuwa wanachimba kihalali ama la na akatoa wito kwa wachimbaji madini kuchukua tahadhali wanapofanya kazi ya uchimbaji kipindi hiki cha mvua.
Awali, wakizungumza na Mwananchi, baadhi ya wachimbaji wamesema wachimbaji hao waliingia mgodini kinyemela kwa nia ya kuchimba madini.
Mmiliki wa mgodi huo, Rahim Mollel amethibitisha kutokea vifo katika mgodi wake.