Serikali mkoani Mara imelitaka Jeshi la Polisi mkoa wa kipolisi Tarime-Rorya kuwakamata ngariba, viongozi wa vijiji, mitaa na wazazi wa watoto 70 waliokeketwa baada ya kurudi nyumbani katika kipindi cha likizo.
Wasichana hao walikuwa wakiishi nyumba salama zilizojengwa na mashirika yasiyo ya kiserikali ili kuepuka kukeketwa kipindi cha Disemba.
Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Mara, Jenerali Suleiman Mzee, wakati wa ziara yake ya kikazi katika vituo vinavyohifadhi watoto hao.
Jenerali mzee amesema kuwa ratiba ya ukeketaji hufanyika Mwezi Disemba ndiyo maana watoto hukimbilia vyumba salama.
Aidha ameongeza kuwa wazazi wa watoto hao walibadili ratiba na kuongeza muda ili kuwafanyia tohara watoto baada ya kurejeshwa nyumbani kipindi cha likizo kutoka kwenye nyumba hizo.