MBUNGE wa Jimbo la Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile amesema kumekuwa na mara mbili ya athari ya mgao wa umeme katika jimbo hilo kutokana na sababu mbalimbali.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram ametaja sababu ya ongezeko la athari kuwa ni upungufu wa uzalishaji wa umeme kitaifa, pia kuzidiwa kwa miundombinu inayoleta umeme Kigamboni.
"Kuna hatua za muda mfupi za kupunguza mzigo kwenye njia ya umeme inayokuja Kigamboni ili umeme usiwe unakatika mara kwa mara," amesema muwakilishi huyo.
Kazi hii inatarajiwa kukamilika ndani ya wiki tatu zijazo. Kukamilika kwa kazi hii, Kigamboni itakuwa inapata umeme kutokana na ratiba zinazotolewa.
"Kuna kazi ya ujenzi wa njia mpya ya umeme ambayo itaifanya Kigamboni kupata umeme mwingi zaidi na kuongeza transfoma eneo la Dege," amesema Ndugulile.
Amesema kazi hiyo itakamilika Februari 2024, na inatarajiwa kuondoa upungufu unaotokana na ongezeko la mahitaji Kigamboni.
"Kama Mbunge naendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu utekelezaji wa miradi yote miwili." Amehitimisha mbunge huyo.