Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai amewataka wasimamizi wa mradi wa ujenzi wa nyumba za walimu katika Shule ya Sekondari Chitego, kutumia fedha zilizotolewa na serikali Sh milioni 171.9 kukamilisha mradi pasipo kisingizio chochote.
Ndugai ambaye ni Spika mstaafu wa Bunge, alisema kuwa fedha zilizotolewa zinatosha kujenga hadi kukamilisha mradi huo, kinachohitajika ni usimamizi mzuri. Amesema wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Chitego kwenye hafla ya uzinduzi wa ujenzi wa mradi wa nyumba za walimu katika Shule ya Sekondari Chitego.
Mradi huo wenye thamani ya Sh milioni 202.2 unatekelezwa na kusimamiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf), ikiwa ni kipaumbele walichoibua wakazi wa kata hiyo ambapo mfuko huo uliahidi kuendelea kutoa fedha za utekelezaji wa miradi kadri jitihada za ukamilishaji wa miradi ya awali zinavyoonekana.