Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Deogratius Ndejembi ameagiza kufungwa kwa taa ili ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Mkoa wa Iringa inayojengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ufanyike usiku na mchana, ili ukamilike haraka na wanafunzi waanze kunufaika.
Ndejembi pia amemuagiza mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kuhakikisha anamsimamia mhandisi wa ujenzi wa shule hiyo ili aongeze idadi ya mafundi, kama ilivyoelekezwa kwenye mkataba.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo, ameeleza kutoridhishwa na kasi ya ujenzi huo kutokana na idadi ndogo ya mafundi.