MENEJA wa Shirika la Umeme Tanzania(Tanesco) mkoa wa Mara, Emmanuel Kashewa ameelezea jinsi ndege anayejulikana kama mwarabu anavyoleta usumbufu katika usambazaji wa umeme mkoani hapa.
Kashewa alisema hairuhusiwi kumuua ndege huyo kwa sababu ya umuhimu wake katika kutunza mazingira. Ndege huyo Musoma wengi humfahamu kwa majina mbalimbali likiwemo hilo la ndege Mwarabu au Msafisha Mazingira.
Alieleza kuwa ndege hao husababisha kukatika umeme kwa dharura, wanapoingia vibaya kwenye kituo kidogo (sub - station) cha kupoza umeme.
Alisema kwenye mashine za kupozea umeme kumewekwa taa zinazotoa mwanga mkali nyakati za usiku, unaosababisha wadudu warukao wakiwamo kumbikumbi na senene kukusanyika kwa kuzingira taa hizo.
“Sasa ndege Mwarabu anapofuata hao wadudu ili awale, hujikuta akisababisha shoti kutokana na ukubwa wa mabawa yake, hata kabla hajafikia taa mabawa yanagusanisha nyaya za laini kati ya mbili hadi tatu,” alisema Kashewa.
Alisema mpaka sasa haijagundulika njia nzuri ya kudhibiti ndege huyo na kwamba kama kusingekuwa
na kifaa cha kulinda njia za umeme (socket brecker), shirika lingepata hasara kubwa sana kwani laini za umeme zingekuwa zinaungua mara kwa mara.
Kashewa alisema tukio hilo linapotokea pamoja na kusababisha shoti ambayo hukata huduma ya umeme kwenye maeneo yote ambayo laini zake zimeguswa na ndege mwenyewe pia hufa palepale.
Kashewa alisema Kituo cha Musoma kinapokea umeme mkubwa, Kv132 na kwamba ukishapozwa kwenye transifoma unapozwa hadi kufikia Kv33 ambazo husambazwa kwa laini za mkoani Mara zikiwamo zinazopeleka umeme kwenye fider (fida) za Majita, Tarime na Musoma mjini.
Alisema inapotokea shoti iliyosababishwa na ndege mwarabu, mara nyingi maeneo yote hayo hukosa umeme mpaka wataalamu wafanye utafiti kubaini chanzo.
Hata hivyo alisema matukio hayo hayatokei mara kwa mara kwa sababu ndege wwarabu, hufuata wadudu siyo taa na kwamba wadudu hutokea zaidi wakati wa msimu wa mvua.