Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communication Limited (MCL), Francis Nanai amewataka wanafunzi waimbaji wa kikundi cha Rising Star Sekondari Great Spalkers (RGS) kuishi kulingana na nyimbo wanazoimba ili kuwa tofauti na wengine.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Agosti 3, 2019 katika uzinduzi wa albamu ya kwanza ya kikundi hicho yenye nyimbo tano katika mahafali ya nane ya shule ya Sekondari Rising Star.
Mbali na uzinduzi wa albamu hiyo ya Alpha na Omega, ziliuzwa CD 230.
Amesema kama wanafunzi hao wanavyosimama na kuimba nyimbo za kusifu na kumtukuza Mungu maneno hayo yakatumike pia kuonyesha tofauti yao na watu wengine.
“Yaishini mnayoyaimba ili muwe tofauti. Walimu pia wasaidieni ili hivi vipaji vinavyoonekana vikuzwe vinaweza kusaidia katika kuboresha maisha na maendeleo mazuri ya shuleni," amesema Nanai.
Awali, mkuu wa shule hiyo, Leticia Herman amesema, “Hapa shuleni tumekuwa tukiwalea vizuri, kufuatilia wanayoyafanya na kuwakemea pale tunapoona wameweka vitu vibaya katika mitandao ya kijamii.”