WAZIRI Mstaafu aliyetumikia awamu ya tatu na ya nne, Mary Nagu ametaka wasichana kujitambua na kuacha matamanio nje ya elimu ili waweze kujikwamua katika mfumo dume na umaskini.
Nagu alisema hayo alipokuwa akizungumza na wahitimu wa Chuo cha Ufundi cha Furahika cha jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Akizungumza katika mahafali ya kwanza yaliyofanyikakatika majengo ya chuo hicho yaliyopo Buguruni Malapa,Nagu alisema wasichana watambue changamoto ya kwanza inayomnyemelea kukatisha ndoto zao ni tamaa nje ya masomo anayochukua.
Aliwataka wasichana walio shuleni kujitambua na kuhakikisha wanalinda ndoto zao za kusaka elimu.
Naye Mwenyekiti wa taasisi ya Furahika yenye chuo hicho, Mohamed Ngwenje alisema mahafali hayo ni ya kwanza na jumla ya wahitimu 22 wa fani mbalimbali za ufundi walipata vyeti vyao vya kumaliza masomo yao.
Hata hivyo Ngwenje aliwataka watoto wa kike kutumia fursa iliyotolewa na chuo hicho kupitia ufadhili wa Mjerumani mama Allen ya kuwasomesha wasichana bure, kupata ujuzi.
Aidha kwa Ngwenje aliwataka viongozi wa sekta yasanaa kushirikiana na chuo hicho ambacho kinatoa pia mafunzo ya muziki ili kuwasaidia vijana wanaomaliza kozi hiyo kwenye chuo hicho kunufaika na ujuzi huo.