Tabora. Mkoa wa Tabora umejipanga kutoa huduma za uhakika pamoja na usalama katika kipindi cha siku tatu kuanzia kesho Jumatano wakati wa jukwaa la fursa za uwekezaji na biashara linalotarajiwa kufunguliwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Akizungumza mjini Tabora wakati wa Ibada maalumu ya kuombea shughuli hiyo leo Jumanne Novemba 20, 2018, Mkuu wa Mkoa huo, Aggrey Mwanri amewahakikishia wageni zaidi ya 500 watakaohudhuria watakuwa salama na kupewa huduma iliyo bora.
Amesema tayari wamezungumza na watoa huduma ya usafiri wa bodaboda kuwa waaminifu kwa wateja wao pale watakaposahau mali zao.
"Kwa wale watakaosahau mkoba kwenye bodaboda watajikuta wanapelekewa mikoba yao na waendesha bodaboda kwani hivyo ndivyo tulivyojipanga," amesema.
Mwanri amesema wamezungumza na waendesha bodaboda kununua pafyumu kila mtu ili wateja wao washangae na kutoisahau Tabora.
Ameeleza wanataka wateja wajiulize kama anapata harufu nzuri katika bodaboda na hakuna atakayenuka kikwapa.
Mkuu huyo wa mkoa amewataka wananchi na wajasiriamali kuitumia fursa hiyo kikamilifu kujiongezea kipato na kupambana na umaskini.
Jukwaa la fursa za uwekezaji na biashara litafanyika kwa siku tatu mfululizo kuanzia kesho na linatarajiwa kufunguliwa na Waziri Mkuu.