Dar es Salaam. Mbunge wa Rwangwa na Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema yapo mambo mengi ya kimaendeleo yaliyofanyika kwenye jimbo lake tangu Rais John Magufuli alipoingia madarakani.
Akizungumza wakati wa ziara ya Rais Magufuli alipotembelea Jimbo la Rwangwa leo Oktoba 15, 2019, Majaliwa amesema Rwangwa ya mwaka 2015 siyo ile inayoonekana sasa kutokana na kuwepo kwa maendeleo.
Amesema Sh27 bilioni zimetolewa kwa wilaya hiyo kwa ajili ya kutekelea miradi mbalimbali ya maendeleo.
“Umetuongezea Sh28 bilioni kwa ajili ya umeme katika vijiji vyote vya Wilaya ya Rwangwa, tunakushukuru sana Mheshimiwa Rais wakati wote tutaendelea kukukumbuka kwa sababu tunaanza kuona mabadiliko makubwa tuliyonayo,” amesema Majaliwa.
Amesema alishapeleka mezani kwa Rais Magufuli ombi la ujenzi wa barabara ya kwenda Nanganga kwa kiwango cha lami baada ya kilometa tano za barabara kutoka Rwangwa mpaka Kitambi kujengwa.
Kuhusu kilimo, Mbunge huyo wa Rwangwa amesema korosho zitakazovunwa katika musimu huu wa kilimo zitabaki wilayani humo baada ya ujenzi wa ghala kubwa la kisasa la kuhifadhia mazao ya kilimo.
Pia Soma
- Ni zamu ya mikoa ya kusini mwa Tanzania maendeleo yake kufufuliwa –Rais John Magufuli
- Magufuli aahidi kuwalipa wakulima wa Korosho jimboni kwa Nape
- Nape ampigia kampeni ‘kiani’ Rais Magufuli
Amesema vyama vya ushirika vilikuwa vinapata shida kusafirisha mazao ya kilimo lakini sasa mazao hayo yatabaki ndani ya wilaya hiyo baada ya ujenzi wa ghala kukamilika.
Amesema ujenzi wa chuo cha Veta kwenye jimbo, hilo kutaongeza ajira kwa vijana kutokana na mafunzo watakayopewa.
Kwa upande wa elimu, Majaliwa amesema wananchi wa jimbo hilo wamesaidia kuchangia jitihada za Serikali za ujenzi wa shule ya msingi itakayoanza kufanya kazi karibuni.