Mbeya. Familia ya marehemu Frank Kapange (22) imelishukuru Gazeti la Mwananchi jinsi lilivyoungana nalo katika kipindi chote cha msiba wa ndugu yao.
Frank aliyefariki Juni 4, 2018 na mwili wake kukaa chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Kanda ya Mbeya tangu wakati huo hadi leo Jumanne Februari 26,2019 ulipochukuliwa na ndugu kwenda kuzikwa.
Kukaa kwa kipindi chote hicho cha miezi nane na siku 22, kulitokana na mvutano wa kisheria baina ya familia na Serikali uliowapeleka Mahakamani.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne baada ya mazishi ya Frank yaliyofanyika kijijini cha Syukula Rungwe jijini Mbeya, msemaji wa familia hiyo, Julius Kapange amesema, “Tayari tumezika mtoto wetu, tulifika Syukula saa sita mchana na tukazika saa saba mchana.”
“Tutaendelea na matanga hapa Kijiji kwa siku tano ila baadhi ya rafiki ambao tulikuja nao huku wamerejea jijini Mbeya.”
Kuhusu Gazeti la Mwananchi, Julius amesema, “Asante sana Mwananchi kwa ushirikiano wenu kwani mlikuwa bega kwa bega na sisi tangu tukio hili lilipotokea mpaka leo tunazika," amesema Julius
Mwili uliokaa mochwari miezi nane Mbeya wachukuliwa na familia yake