Halmashauri tano kati ya saba za Mkoa wa Mbeya zimeagizwa kurejesha Sh 180.9 milioni hasa halmashauri ya Mbarali ambayo inadaiwa Sh79 milioni zilizotakiwa kutolewa mikopo ya asilimia nne za vijana
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Sahili Nyanzabara ametoa agizo hilo leo Jumatano, Septemba 7, 2022 mara baada ya kuwasili katika Wilaya ya Mbarali kukagua miradi sita ya maendeleo.
''Madeni hayo katika hizo halmashauri kabla ya mwenge kuzifikia ziwe zimelipwa serikalini na sio mchezo kwani Serikali inawekeza kwa vijana ili kuweza kujiajiri,'' amesema.
“Sitosema chochote nitakapofika huko kwenye halmashauri ndio tutajua cha kufanya kama fedha hizo bado hazijarejeshwa serikalini na lazima zilipwe,” amesema
Nyanzabara amesema,”Mkuu wa Mkoa, Juma Homera fedha hizo lazima zilipwe kabla hatujazifikia hizo halmashauri tano kati ya saba za Mkoa wa Mbeya.''
Naye Homera amesema Mwenge wa Uhuru utatembelea na kukagua miradi 45 yenye thamani ya Sh 14.7 bilioni na kuzunguka umbali wa kilometa 1014 kwa Mkoa wa Mbeya.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mbarali, Reuben Mfunne amesema kwa Wilaya ya Mbarali utakagua miradi sita yenye thamani ya Sh 1.6 bilioni.