Sumbawanga. Mwanafunzi wa kidato cha nne Shule ya Sekondari Nkomolo wilayani Nkasi, Fredy Pupa (19) amefariki dunia baada ya kuchomwa kisu tumboni na mwenzake wakati wakicheza kamari Akizungumza leo Ijumaa Januari 31, 2020 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Justine Masejo amesema tukio hilo limetokea jana saa 4 usiku katika kitongoji cha Nkomolo wilayani humo.
Amesema Pupa akiwa na mwanafunzi mwenzake wakicheza kamari ulizuka ugomvi baina yao, na kumchoma kisu.
Masejo amesema baada ya kuchomwa kisu alipiga kelele kuomba msaada kwa majirani waliompeleka Hospitali teule ya Wilaya ya Nkasi lakini alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu.
Kamanda huyo amesema mwanafunzi anayetuhumiwa kufanya mauaji hayo anashikiliwa na polisi, atafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.
Katika tukio jingine, Elisha Mgaya amefariki dunia baada ya kutumbukia kwenye kisima wakati akijaribu kuwatoa paka waliokuwa ndani ya kisima hicho.