Muleba. Mwanafunzi wa darasa la pili Shule ya Msingi Kagoma, Belina Bonifasi (9) mkazi wa kijiji cha Kagoma wilayani hapa mkoani Kagera amefariki dunia leo Ijumaa Agosti 24, 2018, ikielezwa kuwa amepigwa na radi.
Akizungumza na MCL Digital leo mzazi wa mwanafunzi huyo, Renatus Pastory amesema mwanae alikutwa na umauti wakati akijiandaa kwenda shule baada ya radi kupiga dirishani.
“Ameungua upande wa kulia wa mwili wake. Alikuwa akiandaliwa chai na mama yake ili aweze kwenda shule,” amesema.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Jeremiah Januari amesema mwanafunzi huyo alikuwa miongoni mwa wanafunzi 115 wa darasa la pili shuleni hapo na kubainisha kuwa wamepokea taarifa za kifo hicho kwa mshtuko.
MCL Digital imewasiliana na ofisi ya kamanda wa polisi mkoa wa Kagera kwa ajili ya taarifa zaidi, kuelezwa kuwa yupo katika kikao.