Serengeti. Mwalimu wa Shule ya Msingi Rung'abure Wilaya ya Serengeti mkoani Mara nchini Tanzania, Godfrey Tarimo (35) amenusurika kifo baada ya kujikata shingo kwa chupa, huku ikidaiwa ni kwasababu ya ugumu wa maisha.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Julai 4, 2019 mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu amesema tukio hilo limetokea jana Jumatano Julai 3, 2019.
Mwalimu huyo amelazwa katika hospitali teule ya Nyerere wilayani humo anakoendelea na matibabu.
Mganga mkuu wa hospitali hiyo,Tanu Warioba amelieleza Mwananchi kuwa Tarimo alifikishwa hospitalini hapo akiwa anavuja damu katika jeraha hilo, akisisitiza kuwa hakupata athari yoyote katika mfumo wake wa upumuaji.
Amesema maelezo waliyoyapata awali ni kuwa mwalimu huyo alichukua hatua hiyo kwa madai ya ugumu wa maisha, kwamba baada ya kupatiwa matibabu ameanza kuzungumza kwa tabu.