Polisi mkoa wa Songwe, wanamshikilia Mwalimu Joseph Mwahenya (34), wa shule ya sekondari Mlowo Day, iliyoko Mbozi kwa tuhuma za kumpiga fimbo, ngumi na mateke mwanafunzi wake wa kidato cha tatu Costantino Mwazembe (18) na kupelekea mwanafunzi huyo kushindwa kusimama, kukaa wala kutembea.
Imeelezwa kwamba alimpiga kutokana na makosa ya utovu wa nidhamu na kwamba mpaka sasa mwanafunzi huyo amelazwa katika hospitali ya wilaya ya Mbozi Vwawa akiendelea na matibabu.
Tukio hilo limetokea Oktoba Mosi, 2022, majira ya saa 6:00 mchana katika shule hiyo na kumuacha mwanafunzi huyo akiwa mwenye maumivu katika sehemu mbalimbali za mwili wake bila kujua hatima ya masomo yake kwani mpaka sasa hajiwezi kwa chochote.
Mganga Mfawidhi wa hospital ya wilaya Mbozi amekiri kumpokea mwanafunzi huyo huku akidai kuwa baada ya vipimo ilibainika kuwa amejeruhiwa katika mishipa ya fahamu.