Same. Mwanafunzi wa kidato cha nne Shule ya Sekondari Kibacha wilayani Same Mkoa wa Kilimanjaro, Happiness Philipo amefariki dunia baada ya kusombwa na maji wakati akivuka mto uliojaa maji kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali nchini.
Akizungumza leo Jumamosi Oktoba 19, 2019 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Salum Hamduni amesema tukio hilo limetokea jana wakati mwanafunzi huyo akivuka mto huo kwenda nyumbani.
"Ni kweli amefariki baada ya kusombwa na maji wakati akijaribu kuvuka mto kuelekea kwenye makazi yao jana jioni,” amesema Hamduni.
Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule amesema baada ya mtoto huyo kusombwa na maji jitihada zilifanyika na mwili wake uliokotwa maeneo ya Kishaa.
"Ni habari za kusikitisha kwa kweli kwa mwanafunzi kusombwa na maji, taratibu zinaendelea atazikwa kesho Jumapili,” amesema.