Dar es Salaam. Mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam zimesababisha adha kwa watumiaji wa barabara katika maeneo mbalimbali jijini humo.
Leo Alhamisi Oktoba 17, 2019 mvua imeanza kunyesha asubuhi huku makamanda wa polisi wakieleza kuwa hadi leo saa 7:45 mchana mvua hizo hazijaleta madhara yoyote.
Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kinondoni, Mussa Taibu amesema hakuna taarifa zozote za madhara alizopokea kutoka mipaka ya wilaya hiyo.
Kamanda wa Polisi Wilaya ya Temeke, Amon Kakwale amesema, “hadi sasa sijapata taarifa za madhara lakini hata nyie vyombo vya habari ni chanzo cha kukusanya taarifa, kama kuna mahali nimesikia mtusaidie."
Mwananchi limepita maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam na kushuhudia baadhi ya mabasi yaendayo haraka (Dart) yakiondoka katika kituo chake eneo la Jangwani ambalo hujaa maji.
Katika eneo la Jangwani hadi leo saa 6 mchana maji yalikuwa yamejaa na kuanza kupita juu ya daraja hali iliyosababisha magari kupita taratibu na kusababisha foleni kutokana na kuanza kutumika kwa barabara moja kwa magari yanayokwenda na kutoka katikati ya Jiji.
Pia Soma
- Wanafunzi 30,675 Tanzania wapata mikopo 2019/20
- Malkia wa Nguvu wa darasa la saba 2019
- Ufaransa, Ujerumani waridhishwa na matumani makubaliano Brexit
- Watu tisa wafariki dunia katika maandamano Guinea