Zaidi ya kaya 65 katika Kijiji cha Imbilili Kata ya Signo wilayani Babati mkoani Manyara, zimekosa makazi baada ya nyumba zao kuezuliwa na upepo mkali ulioambatana na mvua kubwa.
Wakizungumza na HabariLEO jana mjini hapa, wananchi waliokumbwa na adha hiyo juzi walisema kuwa mvua hiyo imeleta madhara makubwa ikiwemo kuumia wakati wakijaribu kunusuru nyumba zao.
Christowelu Mshele alisema ulianza upepo mkali uliokuwa ukikata miti na baadaye mvua ikafuatia hali iliyoleta taharuki na walichokuwa wanafanya ni kunusuru maisha yao mara baada ya nyumba zao kuanza kuezuliwa.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Marcel Lawi alisema jumla ya vitongoji vinne vya kijiji hicho vimeathiriwa na madhara yaliyotokea ni mabati kukunjwa na mazao yaliyokuwa ndani kunyeshewa na mvua.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Babati, Kapinga Franco alisema wameanza kufanya tathmini ya uharibifu uliotokea huku akiwaomba wadau kujitokeza kutoa msaada ili kunusuru kaya hizo.