BARABARA nne kubwa katika kata ya Muungano wilayani Urambo, mkoani Tabora zimeharibika kutokana na mvua kubwa iliyonyesha na kusababisha magari kukwama na mengine kutopita kabisa.
Diwani wa kata hiyo, Shadrakc Manyunya amesema barabara hizo walizozifanyia mrekebisho mwaka wa fedha 2019/2020 zimeharibika vibaya, huku nyingine zikikata mawasiliano kati ya kata hiyo na kata za jirani na kusababisha adha kwa wananchi na wasafiri.
“Barabara hizo zimekatika, zimefanya mashimo makubwa na nyingine kutitia na iwapo Wanyama na magari yatapita yatakwama.”
"Wananchi walichangia fedha za mafuta wakati tunazirekebisha mwaka 2019/2020 na sasa hatuna njia nyingine kwa sababu hata tukisema tulete kijiko bado itakuwa ngumu maana mvua bado zinaendelea kunyesha," alisema.
Diwani huyo alisema kuharibika kwa barabara hizo kumesabisha wamiliki wa vyombo vya usafiri kutafuta barabara nyingine mbadala zinazozunguka maeneo ya mbali na kusababisha kupanda kwa nauli jambo ambalo linaumiza wananchi.
Kata ya Muungano yenye vijiji vitatu ndio pekee yenye barabara inayotoka wilayani Urambo kuelekea tarafa ya Ulyankulu mpaka Kahama, ambapo mabasi ya abiria na magari ya mizigo kwa sasa yamesimama kutoa huduma kutokana na kuharibika kwa barabara hiyo.