Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imewataka wakazi wa mikoa 13 nchini humo kuchukua tahadhari kutokana na mvua kubwa inayotarajia kunyesha.
Taarifa ya TMA iliyotolewa leo Ijumaa Desemba 20, 2019 imeitaja mikoa hiyo ambayo mvua hizo zinatarajia kunyesha kesho Jumamosi ni; Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Singida, Dodoma, Lindi, Mtwara, Rukwa, Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe, Ruvuma pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba, Zanzibar.
TMA imesema athari zinazoweza kujitokeza ni uharibifu wa miundombinu na mali kwa baadhi ya maeneo.
“Baadhi ya makazi kuzungukwa na maji, hatari kwa maisha ya watu kutokana na maji yanayotiririka kwa kasi au maji yenye kina kirefu, ucheleweshwaji wa usafiri, kusimama kwa muda kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi na kijamii,” imeeleza taarifa hiyo
Taarifa hiyo inaeleza, Jumapili ya Desemba 22, 2019 kutakuwa na mvua kubwa kwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara, Rukwa, Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe Ruvuma, Singida, Dodoma pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba.
Jumatatu ya Desemba 23, 2019 mvua inatarajia kunyesha katika baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara, Rukwa, Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe na Ruvuma.
TMA imesema Jumanne ya Desemba 24, 2019 mvua kubwa zinatarajia kunyesha kwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Rukwa, Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe, Ruvuma na maeneo ya kusini mwa mkoa wa Morogoro.