Dar es Salaam. Viashiria vinaonyesha mvua zinazoendelea kwenye ukanda wa Pwani ya Kusini na Kaskazini zitaendelea kwa siku mbili zaidi kuanzia leo Ijumaa Mei 10, 2019, kisha kupungua na kurejea tena katikati ya mwezi huu.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa 10, 2019 jijini Dar es Salaam, meneja wa kituo kikuu cha utabiri cha Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Samwel Mbuya amesema mvua zinazoendelea nchini hususan maeneo ya Pwani ya Kaskazini, Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki na Kanda ya Ziwa Victoria ni sehemu ya mvua za masika.
Amesema mvua hizo zinatokana na kuimarika kwa ukanda wa mvua (ITCZ).
"Mvua za mfululizo katika baadhi ya maeneo ya Pwani ya Kaskazini ikiwamo mikoa ya Tanga, Dar es Salaam na visiwa vya Unguja na Pemba zinatarajiwa kuendelea kwa siku mbili zijazo hadi Jumapili ya Mei 12, 2019.
"Vipindi vya mvua za mfululizo vinatarajiwa kujirudia kuanzia katikati ya Mei 2019," amesema Mbuya.
Amefafanua kuwa mamlaka hiyo itakuwa ikitoa taarifa za
Habari zinazohusiana na hii
mara kwa mara za mwenendo wa mvua hizo katika taarifa zake za utabiri."Pamoja na kwamba mvua za masika zinatarajiwa kupungua maeneo mengi mwishoni mwa Mei 2019, athari
za mvua kubwa zilizonyesha kipindi cha wiki moja mfululizo ukanda wa Pwani ya Kaskazini na visiwa vya Unguja na Pemba zimesababisha kutuama kwa maji na mafuriko.
"Hivyo, kutokana na ardhi kuwa na unyevunyevu mwingi, ongezeko kidogo la mvua linaweza kuendelea kusababisha athari kama zilizokwishatokea wananchi wawe makini," ametahadharisha Mbuya.
Mbuya amesema wananchi wanashauriwa kuendelea kufuatilia taarifa za utabiri kutoka TMA na kuzingatia ushauri na miongozo ya wataalamu ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.