Dar es Salaam. Kamanda wa polisi kikosi cha usalama barabarani, Fortunatus Muslimu ametoa tahadhari kwa madereva wa magari, akiwataka kuzingatia mambo kadhaa katika kipindi hiki cha mvua.
Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Mei 10, 2019 Muslimu amesema ametoa tahadhari hizo kipindi cha mvua kwa maelezo kuwa huambatana na ajali zinazosababisha vifo.
“Kwanza wafuate sheria, waendeshe kwa tahadhari, wafuate alama na michoro ili kutoyapita magari mengine katika maeneo yasiyo sahihi na kuepuka mwendo mkali ambao huenda ukasababisha ajali kutokana na utelezi.”
“Kwa sababu ya ukungu wahakikishe taa zipo sawa muda wote na kabla ya kuanza safari. Wahakikishe magurudumu yapo sawa kwa sababu ya utelezi yakiwa vipara ni hatari zaidi,” amesema Muslimu.
Ameongeza, “Mifumo ya break iwe sawa kwa sababu wakati wa mvua magari huingia maji yanayoweza kusababisha zikafeli, zikiwa imara haitakuwa rahisi kupata hitilafu.”
“Sisi tunaendelea na operesheni nyakua kwa ambao hawatafuata sheria za usalama barabarani ikiwamo na tahadhari hizi nilizozitoa kwa wakati huu wa mvua kubwa.”
Kuhusu maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam ambayo yana foleni kali, Muslimu amesema eneo la Mbezi kuna folani kutokana na ujenzi wa barabara unaoendelea na kubainisha kuwa nchini hakuna daraja lililokatika.