Dar es Salaam. Simanzi imetawala katika familia ya Ally Chande (16) mkazi wa Mwananyamala, Dar es Salaam nchini Tanzania baada ya mtoto huyo kuhofiwa kufa maji katika ufukwe wa Coco.
Chande ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari Kambangwa jana Jumapili aliingia kwenye ufukwe huo kuogelea na hajaonekana tena hadi sasa.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu Julai 15, 2019 shangazi wa mtoto huyo Semeni Chande amesema familia yao imegubikwa na wingu zito kufuatia tukio hilo.
“Jana asubuhi aliaga anakwenda jogging na huwa anafanya hivyo mara kwa mara. Wanaondoka wanakimbia kutoka Mwananyamala hadi Coco Beach ambako hufanya mazoezi.”
“Taarifa tuliyopata ni kwamba baada ya mazoezi yeye na wenzake waliingia kwenye maji kuogelea na baada ya hapo hakuonekana tena, amepotea yeye na rafiki yake ambaye huwa anaondoka naye siku zote,” amesema
Amesema baada ya muda kusonga bila Ally kurejea nyumbani walilazimika kuanza kumtafuta kwa rafiki yake wa karibu ndipo walipogundua kuwa hata huyo rafiki yake hayupo nyumbani.
Pia Soma
- Serikali ya Tanzania yawatangazia neema wakulima wa pamba
- LHRC yajitosa sakata la Mdee, yatoa neno kwa IGP na msajili wa vyama
- Pamba za mamilioni zateketea kwa moto Tanzania
Maue Baba mdogo wa Chonde Ally, Mohammed Ally alisema kwa sasa wanasubiri taarifa yoyote ya kupatikana kwa kijana wao ambaye alipotea katika fukwe ya coco beach.
“Tumeshatoa taarifa kituo cha polisi Osterbay lakini pia wavuvi wamepewa taarifa kuwa watakapomuona watufahamishe,” amesema.
Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kinondoni, Mussa Taibu amesema wanaendelea kutafuta na akipatikana kijana huyo taarifa itatolewa.
“Tunapopata taarifa kama hiyo tunapeleka vituo vyote vya polisi akipatikana taarifa zitatolewa katika kituo wazazi walichotoa taarifa na wazazi watajulishwa,” amesema Taibu.