Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Barabara Vijijini na Mijini (Tarura), Mhandisi Victor Seff, ametoa mwezi mmoja kwa Tarura Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi kukamilisha ukarabati wa Daraja la Ifume.
Mhaindisi Seff ametoa maagizo hayo leo Mei 18, 2022, wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya miradi ya barabara katika Mkoa wa Katavi.
“Daraja hili ni muhimu sana kwa wakazi wa hapa kwa shughuli za kiuchumi, hivyo ni lazima mhakikishe kazi hii inakamilika kwa haraka, ili wananchi wa Kalamsenga na Itunya waweze kusafirisha mazao yao bila kupata usumbufu unaojitokeza kwa sasa, “ amesema Seff.
Amesema Tarura Makao Makuu, itatoa fedha ambazo alielekeza zitumike katika ukarabati wa daraja hilo na kuagiza tathimini ifanyike haraka na maombi ya fedha hizo yatumwe, ili yafanyiwe kazi haraka.
Pia aliwaagiza Tarura wilaya kuhakikisha wanatoa haraka magogo na uchafu wote ulioletwa na mvua na kusababisha kuziba kwa daraja hilo, ili fedha zikija ukarabati ufanyike ndani ya muda wa mwezi mmoja aliotoa.
Naye diwani wa Kata ya Kapalamsenga, Jefu Lameki ameshukuru uongozi wa Tarura kwa kusikia kilio chao, kwani wamekuwa wakipata adha kubwa kutokana na kuharibika kwa daraja hilo.