Arusha. Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amelitaka Baraza Kuu la Waislamu (Bakwata) mkoani Arusha kukemea tabia ya baadhi ya waumini wa dini ya kiislamu kucheza mchezo wa kareti misikitini na kusisitiza kwamba tabia hizo haifai.
Gambo ametoa kauli hiyo leo, Juni 15 mara baada ya ibada ya sikukuu ya Eid iliyofanyika katika uwanja wa michezo wa kumbukumbu wa Sheikh Amri Abeid.
Akizungumza mara baada ya ibada kumalizika Gambo amesema kwamba tabia ya baadhi ya misikiti kufundisha waumini wake mchezo wa kareti ndani ya misikiti haifai na kuwataka Bakwata kukemea tabia hiyo.
“Baadhi ya misikiti kufundisha karate haifai naomba niwapongeze Bakwata kwa kukemea tabia hii na ninawaomba muendelee kulisimamia hili”alisema Gambo
Hata hivyo, alisisitiza kwamba taswira ya waumini wa dini ya kiislamu jijini Arusha kwa sasa imebadilika kwa kuwa hapo awali ilizoeleka kwamba dini hiyo inatafsiri vurugu.
Sheikh Mkuu wa mkoa wa Arusha,Shaaban Bin Jumaa aliwataka waislamu kuhakikisha wanatunza amani ya nchi kila waendako na kujiepusha na vitendo viovu hata baada ya mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Tukio la ibada hiyo liliendana na zoezi la kukabidhi jumla ya vitabu vya dini 3,900 vilivyotolewa na taasisi ya Group Tuelekezane Peponi ambapo vilikabidhiwa kwa waumini mbalimbali wa dini hiyo.