MRADI wa maji kutoka Mto Ruvuma unatarajiwa kuanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/2022 kulingana na upatikanaji wa fedha ikiwa ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati.
Naibu Waziri wa Maji, Maryprisca Mahundi alibainisha hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Mtwara Vijijini, Shamsia Mtamba (CUF), aliyetaka kujua kama serikali ina mpango wowote kupeleka maji ya Mto Ruvuma kwa wananchi wa Mtwara ili kuondoa shida ya maji iliyodumu kwa muda mrefu.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Mahundi alisema mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati na serikali inatarajia kuanza utekelezaji wake katika mwaka wa fedha 2021/22 kadiri ya upatikanaji wa fedha.
“Katika kuhakikisha wananchi wa Mtwara wanaendelea kupata huduma za majisafi na salama, wakati ukisubiriwa utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kutoa maji Mto Ruvuma, Serikali imeendelea kutekeleza kazi mbalimbali za kuboresha huduma za maji kwa wananchi wa Mtwara Mjini,” alisema.
Alisema kazi zinazotekelezwa ni pamoja na uchimbaji wa visima vinne, ufungaji wa pampu tatu, ujenzi wa matanki matatu, ulazaji wa bomba kuu la kilomita saba na bomba la usambazaji maji lenye urefu kilomita 27.
Kwa upande wa vijijini, alisema serikali kupitia Wakala ya Maji na Usafi na Mazingira Vijijini (Ruwasa), inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji 81.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri, miradi hiyo itakapokamilika, itahudumia vijiji 285 na kujenga na kuboresha vituo vya kuchotea maji 1,562 vitakavyonufaisha wananchi zaidi ya 454,375 hivyo kuboresha utoaji wa huduma za maji hadi kufikia wastani wa asilimia 79.91 kutoka asilimia 64 za sasa.