Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, amekataa kuzindua bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya Sekondari Mtekente iliyopo Wilayani Iramba baada ya kubaini kuwa ujenzi wa bweni na jiko vimejengwa chini ya Kiwango.
Bweni hilo limejengwa na Kampuni ya ununuzi wa pamba, Biosustain mkoani humo kwa zaidi ya shilingi milioni 180.
Kufutia hali hiyo amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Iramba kushirikiana na Kampuni hiyo katika kurekebisha maeneo yote yenye kasoro kabla ya shule kufunguliwa.
Amesema ni lazima marekebisho hayo ikiwemo sakafu yarekebishwe ndipo atakapozindua bweni hilo litakalokuwa na uwezo wa kuhifadhi wanafunzi 80.
Dendego amewasisitiza viongozi katika ngazi zote kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika usimamizi wa miradi kama hiyo hata kama ni ya wafadhili ili kazi iweze kufanyika kwa viwango vinavyotakiwa kulingana na thamani ya fedha.