Dar es Salaam. Mkurugenzi mkuu mstaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa (Tiss), Apson Mwang’onda (75) amefariki dunia nchini Afrika Kusini.
Alifariki dunia jana mchana katika Hospitali ya Wilgers iliyopo katika mtaa wa Lynwood, Pretoria.
Mmoja wa marafiki zake wa siku nyingi, Rostam Aziz amethibitisha kutokea kwa msiba huo.
“Nipo hapa Afrika Kusini, ni kweli Mwang’onda amefariki dunia, tunashughulikia safari ya kuurejesha mwili nyumbani na ndani ya siku mbili hizi tutakuwa tumekamilisha,” alisema Rostam kwa kifupi alipozungumza na Mwananchi jana usiku.
Mwang’onda alikuwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kabla ya kuhamishiwa Afrika Kusini alikolazwa kwa takribani wiki tatu mpaka umauti ulipomkuta jana mchana.
Rostam, ambaye ni mfanyabiashara maarufu nchini alisema taratibu nyingine kuhusu msiba huo zitatangazwa baadaye.
Pia Soma
- Benki ya Dunia yaipa Tanzania mkopo wa Sh1tri
- Jafo asema halmashauri itakayogoma kuhamia ofisi za utawala kufutwa
- Hasara, faida kwa wanaokiri makosa uhujumu uchumi
Mwang’onda aliteuliwa katika nafasi hiyo akimrithi Luteni Jenerali Imran Kombe aliyekuwa ameongoza idara hiyo kuanzia mwaka 1983 mpaka 1995.
Mwishoni mwa mwaka jana Mwang’onda alimtembelea Rais John Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu siku hiyo ilieleza kuwa Mwang’onda aliupongeza uongozi wa Rais Magufuli unaochochea kasi ya maendeleo hususani katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo.
Mwang’onda aliitaja baadhi ya miradi kuwa ni Stieglers Gorge, ujenzi wa madaraja na barabara ambazo licha ya kurahisisha usafiri zitasaidia kuondoa msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam.
1. Emilio Mzena (1961 hadi 1975)
2. Dk Lawrence Gama (1975-78)
3. Dk Hassy Kitine (1978-80).
4. Balozi Augustine Mahiga (1980-83)
5. Luteni Jenerali Imran Kombe (1983-1995)
6. Apson Mwang’onda (1995-2005)
7. Othman Rashid (2005-2016)
8. Dk Modestus Kipilimba (2016-2019)
9. Diwani Athuman (2019-)