Dodoma. Halmashauri ya Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma nchini Tanzania imevunja makundi yote ya ‘WhatsApp’ ya waratibu elimu msingi ili kuepuka udanganyifu katika mitihani ya darasa la saba inayofanyika kesho na keshokutwa.
Akizungumza leo Jumanne Septemba 10, 2019 na Mwananchi, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo (DED), Dk Semistatus Mashimba amesema hatua hiyo imechukuliwa kuepuka yaliyojitokeza mwaka 2018 ambapo shule za wilaya zote zilifutiwa matokeo ya mitihani ya darasa la saba.
“Last time magroup haya yalitumika haya magroup katika kuwasiliana. Tumeandika barua kuwataka wavunje hayo magroup, ni kwa waratibu wa elimu tu si kwa watumishi wengine,” amesema.
Katika barua hiyo iliyoandikwa kwa waratibu kata elimu wote Agosti 19, 2019 na kusainiwa na Josephat Ambilikile kwa niaba ya mkurugenzi wa halmashauri hiyo imewataka waratibu elimu kata wote kuvunja makundi hayo.
Makundi hayo ni yale yanayotumika kutoa au kupokea taarifa zozote zinahusiana na utendaji wa taaluma.
Ambilikile amesema pia ofisi imebaini kuwepo kwa makundi ya WhatsApp katika halmashauri hiyo yanayotoa taarifa mbalimbali za kielimu na kijamii.
Pia Soma
- VIDEO: Mahakama yamhukumu mchungaji na wake zake kwenda jela, kulipa faini
- TMA yazungumzia mvua zinazonyesha Dar, yatoa tahadhari
- Jinsi ya kuzuia kumaliza haraka mahaba kwa mwenza wako-1
“Hatua kali za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa dhidi ya kiongozi wa kundi Sogozi (WhatsApp) na wanachama wa kundi husika,” amesema.