Serengeti. Mkurugenzi halmashauri ya wilaya ya Serengeti, Juma Hamsini amemjibu mgombea ubunge wa Serengeti kwa tiketi ya CCM, Marwa Chacha ambaye wakati akiwa Chadema alidai mkurugenzi huyo ni mwizi mbele ya Rais John Magufuli.
Akizungumza leo Jumanne Oktoba 30, 2018 Hamsini amesema kitendo cha Chacha kutamka maneno hayo mbele ya kiongozi mkuu wa nchi, ni ukosefu wa fadhila.
Septemba 6, 2018 katika ziara ya Rais Magufuli wilayani Serengeti, Chacha wakati huo akiwa mbunge wa Serengeti kwa tiketi ya Chadema, alimshukia mkurugenzi huyo akidai kuwa amefuja zaidi ya Sh500milioni.
Septemba 27, 2018 Chacha alihama Chadema na kujiunga na CCM ambapo leo kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya chama hicho tawala kimempitisha kuwania ubunge wa Serengeti. Wengine waliopitishwa kuwania ubunge na majimbo yao kwenye mabano ni Pauline Gekul (Babati Mjini), James Mallya (Simanjiro) na Joseph Mkundi (Ukerewe).
Hamsini ametoa kauli hiyo leo wakati akizindua mradi wa Mazingira na Usafi Tanzania (Finish Fort) katika kata 11 huku akibainisha kuwa wakazi wa wilaya hiyo hawana fadhila.
"Mfano Marwa mbele ya Rais alinitukana mimi kuwa ni mwizi huku ni kukosa fadhila na hata miradi inayoletwa hapa hawana fadhila badala yake viongozi huzusha uongo," amesema.
Hamsini amesema hakuwepo ila sasa ndio amerejea na atakuwa msimamizi wa uchaguzi mdogo wa Serengeti ambao Chacha anagombea kwa tiketi ya CCM.