Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mara, Langaeli Akyoo ameitaka TAKUKURU kuingilia kati ubadhirifu wa fedha Shilingi milioni 102 za kitanzania, fedha za ujenzi wa nyumba ya mwalimu mkuu (two in one) katika shule ya msingi Nyangoto ambazo zilitolewa na mgodi wa North Mara (CSR).
Akyoo ameyasema hayo katika kikao cha majumuisho ya ziara ya utekelezaji miradi huku jengo hilo likikadiriwa kutokuwa na ubora pamoja na kutomalizika kwa muda uliopangwa kwa takribani miaka minne katika halmashauri ya Tarime Vijijini.
Amesema baadhi ya watumishi wa serikali wameonekana kutengeneza mazingira magumu kwa viongozi wa chama, na chama kutupiwa lawama kuwa hakitekelezi wajibu wake kwa wananchi.
"Ninaiagiza TAKUKURU mkoani hapa kuhakikisha inafuatilia suala hili na kulipatia ufumbuzi na ikiwezekana fedha zilizoliwa ziweze kurejeshwa mara moja" amesema Akyoo.