Njombe. Wananchi kutoka maeneo mbalimbali mkoani Njombe wameshiriki shughuli ya kuaga miili ya polisi watatu waliofariki katika ajali ya gari mkoani humo.
Polisi hao walifariki dunia jana alfajiri Jumatatu Februari 3, 2020 baada ya gari walilokuwa wamepanda kugongana na basi la kampuni ya Sharon.
Akizungumza katika shughuli hiyo leo Jumanne Februari 4, 2020 mkuu wa Mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka amesema Serikali imepoteza nguvu kazi ya Taifa kwa kuwa askari hao walikuwa na umri mdogo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Hamis Issah aliwashukuru wakazi wa Njombe kwa kujitokeza kwa wingi pamoja sambamba na kutoa michango kuhakikisha askari hao wanasafirishwa katika maziko.
Watu mbalimbali walishiriki ibada ya kuaga miili ya askari hao ambao ni Marianus Hamissi, Michael Mwandu na Henry Soka.