Ukerewe. Licha ya kivuko cha Mv Nyerere kuzama majini zaidi ya saa 48 zilizopita wilayani Ukerewe, Alphonce Charahani, mhandisi wa kivuko hicho ameokolewa leo asubuhi akiwa hai.
Kivuko hicho kilizama juzi mchana, lakini Charahani ameokolewa leo Jumamosi Septemba 22, 2018 saa 4:45 asubuhi akiwa hai.
MCL Digital iliyopo eneo la tukio imeshuhudia mhandisi huyo akitolewa akiwa hai na kukimbizwa Kituo cha Afya cha Busya kilichopo katika Kisiwa cha Ukara.
Akizungumza na MCL Digital, mmoja wa wazamiaji, Daniel Kondoyo amesema tangu juzi Septemba 20, 2018 kilipozama kivuko hicho kila walipokuwa wakigonga walisikia mtu mwingine akigonga kwa ndani.
Baadhi ya wazamiaji wanaoopoa miili wamesema Charahani alikuwa amejipaka oili mwilini ambayo wameielezea kuwa husaidia maji yasiweze kupita katika vinyweleo.
Kandoyo amesema kutokana na hali hiyo huenda aliyekuwa akigonga kwa ndani ni Charahani.