Dar es Salaam. Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani imepiga marufuku mgomo wa madereva wa mabasi yaendayo mikoani.
Tamko la kupiga marufuku mgomo huo limetolewa leo Mei 14, 2019 na Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Fortunatus Muslim, baada ya kukaa na kujadiliana na wadau wa usafirishaji ikiwamo Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu (Sumatra), Chama cha Wamiliki wa Mabasi yaendayo mikoani (Taboa) na Chama cha Madereva wa Mabasi yaendayo ya Masafa Tanzania.
Hatua hiyo imetokana na kuwapo kwa taarifa katika mitandao ya kijamii zilizoanza kusambaa tangu Jumapili iliyopita zikihamasisha kufanyika kwa mgomo huo kuanzia kesho Jumatano Mei 15, 2019.
Akitoa tamko hili kwa waandishi wa habari katika kikao cha pamoja na wadau wa usafiri huo, Kamanda Muslimu amesena mgomo huo ni batili kwa kuwa haujafuata taratibu za kisheria.
Pia, Muslimu amesema mambo wanayoyalalamikia yako mahakamani ambako tayari wamefungua kesi na kwamba, mengine yanafanyiwa kazi na mamlaka husika.
Amesema baada ya kukutana na kujadiliana na wadau wamekubaliana kuwa, kwa kuwa kero zinazolalamikiwa ziko mahakamani hivyo ni vyema watoe nafasi kwa Mahakama iweze kuzishughulia na haitakuwa vizuri kufanya mgomo kabla Mahakama haijamaliza kazi yake.
Pia Soma
- Mkapa, Profesa Rubaratuka waula tena
- Tiger Woods ashtakiwa kwa shtaka la ajabu
- Maradona kutikisa Tamasha la Filamu Cannes
"Hivyo hatutegemei kuwa kesho huduma za usafiri hazitatolewa, mwenyekiti wao Shaaban Mdem wamesema hawana taarifa za kuwapo kwa mgomo huo.”
Viongozi hao wamesema hawajahusika wala kutaarifiwa kuwapo kwa mgomo huo na kwamba, hata wao taarifa hizo walizisikia na kuziona tu kwenye mitandao ya kijamii.
Kwa hiyo, wamewataka madereva kusitisha mgomo huo na kuendelea na utoaji huduma wakati malalamiko yao yakifanyiwa kazi na Mahakama pamoja na mamlaka nyingine zinazohusika na usimamizi.