Mvua zinazoendelea kunyesha katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zinaelezwa kuwa zimechangia kuongezeka kwa kiasi cha maji katika bonde la mto Ruvu na hivyo kupunguza mgao wa maji.
Sambamba na mvua, operesheni zilizofanywa za kuwaondoa walioingilia mto huo na kuchepusha maji, zimechangia kuongeza maji yanayokwenda Dar es Salaam.
Hayo yameelezwa leo na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Nadhifa Kemikimba wakati akifungua mkutano wa wadau wa maji kujadili namna ya kutunza bonde la mto Ruvu ambalo ni chanzo kikuu cha maji kwa Jiji hilo.
Nadhifa amesema hali ya maji ilivyo sasa ni tofauti na ilivyokuwa wiki tatu zilizopita hadi kusababisha kutangazwa kwa mgao na kwamba mgao umepungua kwa kiasi kikubwa na kuna maeneo yalikuwa yanapata maji mara tatu kwa wiki lakini sasa kila siku maji yanapatikana.
Advertisement “Kwa kiasi kikubwa inahitajika elimu ya matumizi ya maji. Ni kweli yameanza kuongezeka lakini sio kwa matumizi ya kumwagilia ndio maana bado hatujaruhusu shughuli za umwagiliaji na matumizi mengine yasiyo ya kibinadamu,”
Kwa upande wake, Kaimu Ofisa wa Maji Bonde la Wami Ruvu, Mhandisi Bariki Mmasi amesema kwa sasa kiasi cha maji kinachopita kwenye kipimo ni lita 10,000 kwa sekunde huku mahitaji yakiwa lita 12,900.
“Kulingana na wadau wetu tuliowapatia vibali maji yanayohitajika ni lita 12,900 kwa hiyo kiasi tulichonacho tunaona kwa matumizi ya binadamu tumeanza kuwa vizuri bado hatujakaa sawa kuruhusu matumizi mengine,” amesema Mmasi.