Mganga wa kienyeji mkazi wa kijiji cha Sungamile Kata ya Mwalugulu Halmashauri ya Msalala mkoani Shinyanga, Ngusa Jiramba(58) aliyeuawa Januari 20 mwaka huu pamoja na mke wake Bugumba Mahola(52) kwa kucharangwa mapanga na shoka amezikwa akiwa amekaa kama sehemu ya mila zao.
Mtoto wa marehemu Simbira Ngusa ambae akisimulia tukio la mazishi ya baba yake amesema, Januari 20 walivamiwa na watu wasiojulikana na kuwauwa wazazi wake kwa kuwacharanga mapanga na shoko vichwani kwa madai ya kutaka fedha.
Amesema, kiasi walichochukua ni kiasi cha Sh. 700,000 ambacho pia walidai hakitoshi kununua ng’ombe na haya waliyasikia wakati wa majibizano baina ya wazazi wake na watu hao kabla ya kufanya mauaji na kuomba serikali kuwachukulia hatua wote waliohusika kwenye mauaji hayo.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP.Janeth Magomi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kudai kuna baadhi ya wanafamilia wanashikiliwa na jeshi la polisi na upelelezi unaendelea na wale watakaobainika kuhusika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.