Shinyanga. Mbunge wa zamani wa Meatu mkoani Simiyu, Jeremia Mlyambate amefariki dunia leo Jumanne Novemba 20, 2018 wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya wilaya ya Kahama.
Mtoto wa marehemu, Andrew Mlyambate amesema baba yake alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi tangu mwaka 2013 na amekuwa akipatiwa matibabu katika hospitali kadhaa ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Bugando (BMC) jijini Mwanza.
Amesema baba yake ambaye pia amewahi kuwa mjumbe wa Bodi ya Shirika la Hifadhi ya Taifa (Tanapa) atazikwa Novemba 22, 2018 nyumbani kwake kijiji cha Mwabuzo wilayani Meatu.
"Wakazi wa Shinyanga na vitongoji vyake watapata fursa ya kutoa heshima ya mwisho katika ibada fupi itakayofanyika mjini Shinyanga kuanzia saa 4:00 asubuhi kesho Novemba 21, 2018," amesema Andrew
Marehemu Mlyambate alikuwa mbunge wa Meatu kati ya mwaka 1990 hadi 2005.