Mikoa ya Mbeya na Dodoma itaanza kufungua utepe wa mashindano ya urembo ya Miss Tanzania mwaka huu.
Mkurugenzi wa Kampuni ya The Look, Basila Mwanukuzi amesema mikoa mingine iliyobaki itafanya mashindano yake Julai 7.
Mkoa wa mwisho kupata warembo wake kwa ajili ya kusaka warembo wa shindano la Taifa ni Kinondoni ambao utafanya mashindano yake Julai 20.
Mwanukuzi alisema kuwa baada ya mashindano ya mikoa kumalizika mashindano ya Kanda yataanza na Kanda ya kwanza kufanya shindano lake itakuwa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, ikihusisha mikoa ya Rukwa, na Mbeya Julai 13.
Kanda ya Mwisho kufanya shindano lake itakuwa Kanda ya Mashariki itakayojumuisha mikoa ya Pwani na Morogoro na itafanya shindano lake mjini Morogoro Agosti 4.
Baada ya mashindano ya mikoa na Kanda, washiriki wapatao 25 wataingia katika kambi ya Taifa kwa muda wa mwezi mmoja kujiandaa kwa fainali za Taifa ambayo tarehe yake itatangazwa hapo baadaye.
“Uongozi wa Kampuni ya The Look Company Limited una hamasisha wadau wa tasnia ya urembo kujitokeza kwa wingi kuhudhuria mashindano haya ambayo kwa mwaka huu 2018 yanakuja kivingine,” alisema Mwanukuzi .