Serengeti. Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu nchini Tanzania, Anthony Mavunde ameitaka kampuni ya Grumeti Reserve kulipa faini ya Sh1.4 milioni baada ya kubainika wafanyakazi wake kufanya shughuli zao bila kuvaa mavazi ya usalama kazini.
Mavunde ameigiza Mamlaka ya Usalama Mahala pa Kazi (Osha) kuhakikisha wanachukua faini hiyo ya Sh1.4 milioni kwa kampuni hiyo inayojishughulisha na masuala mbalimbali, yakiwemo ya utalii katika mapori ya akiba kijiji cha Makundusi wilayani Serengeti Mkoa wa Mara.
Akizungumza leo Jumanne Oktoba 22, 2019 baada ya kuitembelea kampuni hiyo, Mavunde amesema kwa mujibu wa sheria na taratibu za kazi ni wajibu wa mwajiri kuhakikisha wafanyakazi wake wanafanya kazi katika mazingira salama.
Mavunde amesema katika ziara hiyo amegundua zaidi ya wafanyakazi 25 wa kitengo cha ujenzi na ufundi wanafanya kazi bila kuwa na vifaa hivyo na baadhi wakiwa wamefanya kazi katika hali hiyo kwa miaka mitano.
“Nimekaa saa moja tu hapa lakini nasikia vumbi limejaa kifuani, sasa hawa watu wamefanya kazi hapa wengine hata miaka minane bila kuwa na vizuia vumbi wala mabuti, hivi hii ni haki kweli,” amehoji Mavunde.
Mbali na kuwataka kulipa faini, Mavunde ametoa muda wa siku saba kwa kampuni hiyo kuhakikisha vifaa vya kazi vinapatikana na wafanyakazi wote wanapatiwa.
Pia Soma
- Tanzania yapendekeza Kiswahili kupandishwa hadhi Umoja wa Mataifa
- Watumishi wa Serikali ya Tanzania wadaiwa kutolipa madeni NHC
- Watano mbaroni polisi wakipambana na madereva Bajaj Iringa
Amesema walipobaini kutokuwepo kwa vifaa hivyo walitoa taarifa kitengo cha utawala Agosti, 2019, kwamba muda wowote watapokea vifaa hivyo.