Dar es Salaam. Siku moja baada ya Rais wa Tanzania, John Magufuli kuzindua barabara ya Tunduma- Sumbawanga na kueleza kuwa ina matuta mengi hatua zimeanza kuchukuliwa kuhakikisha yanapunguzwa.
Waziri wa Ujenzi, Isack Kamwele amesema tayari ameiagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kufanyia kazi changamoto hiyo na kuyapunguza.
Akizungumza leo Jumatatu Oktoba 7, 2019 wakati wa uzinduzi wa mradi wa maji mkoani Rukwa Kamwelwe amesema ameshatoa maelekezo barabara hiyo yenye matuta 222 kupunguzwa.
Kuhusu uwanja wa ndege wa Sumbawanga Kamwelwe amesema tayari Serikali imeshalipa fidia ya Sh3.7 bilioni na taratibu za kifedha zitakamilika mwezi ujao kisha ujenzi wake kuanza mara moja.