Tanga. Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amemuagiza Mkurugenzi wa halmashauri ya Jiji la Tanga kufanya uchunguzi na kisha kuwachukulia hatua waliohusika na kujengea matofali badala ya ndono kwenye madirisha ya majengo ya shule ya Sekondari Galanos.
Naibu Waziri huyo amefanya ziara ya kushtukiza shuleni hapo jana usiku Jumapili Agosti 25,2019 na kubaini madirisha hayo yamejengewa na matofali badala ya nondo kama ilivyooneshwa kwenye mchoro wa majengo hayo ambayo yanatarajiwa kugharamia Sh900 milioni hadi kukamilika.
Akizungumza baada ya kukagua majengo hayo yanayokarabatiwa chini ya mpango wa Serikali wa kukarabati shule kongwe nchini, Ole Nasha alisema mchoro unaonesha majengo hayo yanatakiwa kukarabatiwa kwa kutumia nondo lakini amekuta yamejengewa matofali.
“Kuna mapungufu makubwa na ya makusudi kwanza sijapata majibu kwa nini zisitumike nondo kama ilivyooneshwa kwenye mchoro na badala yake yakajengewa matofali lakini pia nimetilia shaka uimara wake,” alisema Ole Nasha.
Kwa mujibu wa maelezo ya Naibu Waziri huyo ni kwamba dosari katika ukarabati shule hiyo ambao kwa sasa umefikia asilimia 40 umesababisha mvutano baina ya bodi ya shule ambayo imeonyesha kutoridhishwa na mkandarasi.
“Nimemuagiza Mkurugenzi wa Jiji kufanya uchunguzi na achukue hatua kwa kila aliyehusika lakini mhandisi wa Jiji hawezi kukwepa kwa sababu ndiye aliyeshauri kubadilishwa kwa ujenzi huu wakati yeye ndiye aliyehusika na kuchora mchoro huo,” alisema Ole Nasha.
Pia Soma
- Wadau wa usafiri Mwanza wasusia kikao, waitaka mamlaka kujipanga
- Viongozi ACT Wazalendo, mwandishi wa habari wapewa dhamana
- Teknolojia ya mawasiliano ni nguzo muhimu ya ukuaji wa biashara nchini