Butiama. Watu wa kada mbalimbali leo Jumatatu Oktoba 14, 2019 wamefika nyumbani kwa mwalimu Julius Nyerere, Mwitongo Butiama kushiriki ibada na sala maalumu kukumbuka miaka 20 ya kifo cha Rais huyo wa kwanza wa Tanzania.
Watu hao wamekusanyika kuanzia asubuhi leo katika ibada ya kumwombea Nyerere iliyofanyika Kanisa Katoliki Musoma na baadaye kufuatiwa na sala maalum iliyofanyika nyumbani kwake.
Miongoni mwa wanaojumuika ni wazee maarufu wa Butiama (Watiama) waliokuwa wakiishi, kucheza, kula na kulima pamoja na mwalimu Nyerere.
Akitoa salaam za Mkoa wa Mara katika ibada ya kumwombea Mwalimu Nyerere, mkuu wa Mkoa huo, Adam Malima amesema pamoja na wazee hao wa Butiama, tukio maalum la kuzungumzia maisha ya Nyerere litajumuisha viongozi wastaafu waliofanya kazi pamoja na kiongozi huyo.
Miongoni mwao ni waziri mkuu mstaafu, Joseph Warioba; makamu mwenyekiti wa CCM, Phillip Mangula na waziri wa zamani, Stephen Wasira
Wakitoa salaam kwa nyakati tofauti katika ibada hiyo, Warioba, Mangula na Wasira wamewaasa Watanzania kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa kulinda utu, haki na usawa.