Dar es Salaam. Zikiwa zimesalia saa chache kabla ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kufungwa kwa laini za simu ambazo hazijasajiliwa kwa alama za vidole, mamia ya wananchi wamejitokeza katika ofisi za Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) wilaya ya Ilala Dar es Salaam huku wakilalamikia kasi ndogo ya utoaji huduma.
Nje ya ofisi za Nida zilizopo Ukonga, usajili wa laini za simu pia unaendelea huku mawakala nao wakilalamikia tatizo la mtandao, jambo linalokwamisha usajili wa laini za simu kwa haraka na muda mfupi.
Mwananchi limeshuhudia baadhi ya watu ambao wamefanikiwa kupata namba zao za kitambulisho kabla ya ukomo wa muda kufika leo Jumatatu Januari 20, 2020 saa 5.59 usiku, wakiwa na furaha kwa kukamilisha mchakato huo.
"Aisee nimepiga kambi hapa tangu saa moja, watu walikuwa wengi lakini nashukuru leo nimekamilisha. Ingawa bado sijapata kitambulisho lakini angalau naweza kusajili laini yangu. Changamoto hapa ni kasi ndogo ya watendaji wa Nida," amesema Fadhili Mohammed, mkazi wa Majumba Sita.
Habari zinazohusiana na hii
- Wananchi Mwanza wanavyosotea vitambulisho vya Taifa
- Machungu ya laini za simu kuzimwa
- Makonda adai wasio na vitambulisho vya Taifa Dar wanaendekeza umbea
- Wakazi Dar watakiwa kujitokea viwanja vya Zakhem Mbagala kusajili laini za simu
"Mi hata sielewi kama nitaipata hiyo namba leo au la! Wakinifungia laini zangu, basi, nitaendelea kuja mpaka nipate hiyo namba. Nimeacha shughuli zangu kwa ajili ya kushughulikia hili suala," amesema mwanamke huyo.
Mmoja wa mawakala wanaosajili laini za simu, Ombeni Mwanjisi amesema usajili unafanyika kama kawaida lakini wanakabiliwa na changamoto ya mtandao ambao unakuja na kuondoka.
"Mtandao sio mzuri, tunatumia muda mrefu kusajili mtu mmoja. Baadhi ya kampuni za simu kama Halotel, mtandao uko vizuri lakini mingine lazima usubiri," amesema wakala huyo wakati akiendelea na usajili wa laini za simu kwa alama za vidole.
Mkazi wa Tabata Dar es Salaam, Ibrahim Abdallah amesema ameshindwa kusajili laini yake kutokana na mtandao wa kampuni ya simu kuwa chini.
“Mimi jana nimeshinda kwa wakala wa mtandao wa Vodacom toka asubuhi hadi jioni lakini sikusajili kwa sababu mtandao ukiwa unasumbua na leo nimekwenda hali ni ile ile kwa hiyo Serikali inapaswa kuliona hili kwani si makosa yangu ila ni mtandao,” amesema