Geita. Watoto watatu wamezaliwa katika Hospitali ya Mkoa wa Geita na wawili wakiwa wameungana eneo la kifuani.
Watoto hao ambao wote ni wa kike, walizaliwa Jumapili ya Machi 17, 2019 Saa 10 jioni.
Imeelezwa kuwa mtoto mmoja alizaliwa kwa njia ya kawaida na wawili walioungana walizaliwa kwa njia ya upasuaji.
Daktari wa wa maradhi ya wanawake hospitalini hapo Joseph Makuma, ameliambia Mwananchi leo Machi 19, 2019 kuwa Machi 17 walipokea wajawazito wawili kutoka Wilaya ya Nyang’hwale waliopatiwa rufaa baada ya kugunduliwa wanakiwango kidogo cha damu.
Amesema muuguzi aliyekuwa zamu aliwapokea wajazito hao lakini Theodora Wilson alikuwa na uchungu mkali na alisaidiwa kujifungua na kufanikiwa kujifungua mtoto wa kwanza wa kike.
“Baada ya kumzalisha, nesi alishtuka kwakuwa tumbo la mama lilibaki kuwa kubwa, aliponiita nije kumtazama na kumpima nikagundua bado ana watoto tumboni,” amesema Dk Makuma.
Amesema alipompima njia alikuta mtoto ametanguliza mkono jambo ambalo ni hatari na aliamua kumfanyia upasuaji
“Tulifanimiwa kumpasua na kumtoa mtoto, lakini sikujua kama wameungana nilimshika mtoto mguu nikamnyanyua ndio nikaona wametoka wawili wameungana wakiwa na kilo 4.5 na wana afya njema,” amesimulia daktari huyo.
Kwa mujibu wa daktari, watoto wote wawili wana afya njema na kila mmoja amekamilika viungo na anajitegemea.
Mama wa watoto hao, Theodora William ambaye ni mwalimu wa shule ya msingi, amesema anamshukuru Mungu kwa uzao huo na kuomba Mungu awawezeshe madaktari kuwatenganisha watoto wake salama.
“Mimi naona ni kusudio la Mungu kwa kuwa amenipa, anajua atakavyowasaidia siangalii tatizo kwakuwa najua lipo kusudio la Mungu,” amesema.
Mwalimu huyo ameiomba Serikali kumsaidia gharama za kuwatenganisha watoto hao nakuomba kuongezewa muda wa likizo ya uzazi kusudi awatunze wanawe.
Watoto hao wamesafirishwa kwenda hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa uchunguzi zaidi.