Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesema malimbikizo ya madeni ya kodi ya majengo Wilaya ya Kinondoni mwaka 2018/2019 yamefikia Sh1.9 bilioni.
Akizungumza leo Ijumaa Januari 31, 2020 katika uzinduzi wa kampeni ya ulipaji kodi ya majengo kwa mwaka wa fedha 2019/2020, meneja wa TRA Wilaya ya Kinondoni, Masawa Masatu amesema madeni hayo ni sehemu ya malimbikizo ya miaka mingi ya nyuma.
Amesema wakati kukiwa na malimbikizo hayo, wilaya hiyo inatakiwa kukusanya Sh5.7 bilioni kwa mwaka wa fedha 2019/2020 na mpaka sasa wamefikia asilimia 50 ya makusanyo yote.
“Mwaka uliopita tumefunga mwaka tukiwa na malimbikizo ya Sh1.9 bilioni na ambao hawajalipa madeni yao wameendelea kulipa,” amesema Masatu.
Mkuu wa wilaya Kinondoni, Daniel Chongolo amesema TRA wamepewa jukumu la kukusanya kodi ya majengo manispaa na katika halmashauri tangu Serikali ilipoihamishia majukumu hayo.
“Tunazindua rasmi zoezi la uhamasishaji jamii kulipa kodi ya jengo kwa mwaka 2019/20 itakoma mwezi wa sita, wananchi hawajahamasika vya kutosha Rais alitoa msamaha na kupunguza kiwango cha kodi ya majengo mpaka kufikia Sh10,000 kwa jengo la kawaida la chini na mwenye ghorofa analipa Sh50,000 kwa ghorofa moja,” amesema.
Pia Soma
- Homa ya tamasha la Sauti za Busara yazidi kupanda Zanzibar
- Pizza Hut na KFC yafungua mgahawa wa 14 Tanzania
- Sita wakiwamo maofisa forodha kortini tuhuma za utakatishaji wa mamilioni
“Tunazindua kampeni hii leo ifikapo 30 Juni wananchi wote wawe wamelipa. Tutafuatilia kila kata ili kuhakikisha kila mwanakaya amelipa tusisubiri deadline watu wote walipe kwa wakati. Wito wangu kwa wakazi wa Kinondoni anayemiliki jengo kwenda kulipa ili kuondoa shida za baadaye,” amesema.