Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amezitaka manispaa za Mkoa wa Dar es Salaam na Jeshi la polisi mkoani humo kurejesha kompyuta 30 alizowapatia ifikapo Septemba 30, 2019 ikiwa hazitumiki kama ilivyokusudiwa ili awapatie Idara ya Uhamiaji.
Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Agosti 29, 2019 muda mfupi baada ya kuzindua mkakati wa kudhibiti wahamiaji haramu Mkoa wa Dar es Salaam.
Amesema amewahi kutoa kompyuta nane kwa kila manispaa ya Mkoa huo kutatua changamoto za utoaji wa vibali vya ardhi lakini tangu wakati huo hadi sasa hajapata mrejesho kama zinafanyiwa kazi iliyokusudiwa.
Amebainisha kuwa kama zinafanyiwa kazi ambayo haijakusudiwa wazirejeshe ili awapatie uhamiaji.
Kwa upande wa polisi, Makonda amesema kila Wilaya aliipatia kompyuta 20 ili kufunga mfumo wa kutoa mawasiliano ambao utaonyesha mahabusu walioingia na kutoka polisi.
Amesema akipita katika vituo hivyo hazioni kompyuta hizo, badala yake anakutana na vitabu, kusisitiza kuwa kama hazitumiki zirudishwe.