Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema mwaka 2020 atamkabidhi Rais John Magufuli mkoa huo ukiwa na viongozi wa kuchaguliwa wanaotokana na CCM.
Mkoa wa Dar es Salaam kwa sasa una baadhi ya viongozi wa kuchaguliwa wanaotokana na vyama vya upinzani, wakiwemo madiwani, wabunge na mameya wa Chadema na CUF.
Makonda ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Desemba 20, 2018 katika hafla ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa daraja la Selander na barabara unganishi.
Amesema kwa maendeleo ambayo yamefanyika kwenye mkoa huo ana uhakika wapinzani wengi wataunga mkono juhudi hizo.
“Kama mambo yakiendelea hivi mwaka 2020 nitakukabidhi Mkoa ukiwa na wabunge, madiwani na mameya wote wa CCM,”
“Wanaotaka demokrasia ya kutembea wasubiri tumalize kujenga barabara ili tukimaliza ndio watembee kwenye barabara nzuri,” amesema Makonda.
Makonda amedai kitendo cha wabunge wa vyama vya upinzani kuhamia CCM ni toba na bado wapo wabunge na madiwani hadi sasa wanaulizia kujiunga na chama hicho.
“Baada ya lile tangazo linaloeleza mwisho wa kujiunga CCM alilolitoa Polepole (Humphrey- Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM) baadhi ya madiwani wameniuliza kama ndio mwisho itakuwaje? Nimewaeleza wasubiri kama kutakuwa na usajili wa dirisha dogo,” amesema Makonda.